Mkurugenzi Mkuu Taasisi ya Elimu Tanzania Dkt Aneth Komba amewataka walimu wanaofundisha ngazi ya maandalizi na msingi kufuata misingi ya mtaala mpya wa ujenzi wa umahiri ili lengo la Serikali la kuwa na Elimu bora liweze kufikiwa
Akifungua mafunzo ya utekelezaji wa mtaala mpya unaozingatia ujenzi wa umahiri kwa walimu wa darasa la nne huko kituo cha Walimu Dunga wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja amesema hatua hiyo itasaidia kufikia malengo ya kubadilishwa kwa mtaala kutoka ule wa nadharia na kuja wa vitendo.
Amesema azma ya Serikali ya kubadisha mtaala huo ni kuona unaendana na mazingira halisi ya Zanzibar hali itakayosaidia wanafunzi watakapomaliza elimu ya msingi kuwa na uelewa .
Amesema somo la sanaa za ubunifu na michezo limekwenda kuakisi dhana ya uchumi ambao ndio malengo makuu ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Aidha Mkurugenzi huyo ameipongeza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kupitia Taasisi ya Elimu ya Zanzibar kwa hatua iliyofikia ya kuanza kutumia mtaala mpya unaokwenda kuijenga upya Zanzibar kielimu.
Mapema Meneja wa Utafiti na Udhibiti Ubora Taasisi ya Elimu ya Zanzibar Nd Faridu Muhammed Wakil amesema mtaala wa maandalizi na msingi unaokwenda kutumika kwa baadhi ya madarasa umeakisi malengo ya jamii pamoja na kufanyiwa upembuzi yakinifu.
Taasisi ya Elimu ya Zanzibar kuanzia tarehe 20/2/2023 umeanza kutumia mtaala mpya unaozingatia ujenzi wa umahiri na tayari walimu wa ngazi ya maandalizi mwaka wa kwanza darasa la kwanza tayari wameshapatiwa mafunzo na kwasasa mafunzo yanaendelea kwa darasa la nne.